
Na Mwandishi Wetu
DAR
ES SALAAM — Kampuni ya teknolojia ya kifedha ya Black Swan-Tanzania
imeingia kwenye orodha ya kampuni 25 bora zinazochipukia barani Afrika
kwa mwaka 2026 iliyotolewa na taasisi kubwa ya habari za fedha duniani,
Bloomberg.
Black
Swan, kampuni iliyosajiliwa Tanzania na inayojihusisha na huduma za
kifedha kupitia teknolojia ya akili mnemba (AI), imetambuliwa kutokana
na mchango wake wa kurahisisha upatikanaji wa mikopo nafuu na ya haki
kwa Waafrika ambao bado hawajahudumiwa kikamilifu na mifumo rasmi ya
kifedha.
Orodha
hiyo ya Bloomberg hutambua kampuni kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika
zinazotatua changamoto muhimu kwa kutumia teknolojia na ubunifu wenye
matokeo chanya katika jamii na uchumi.
Kupitia
teknolojia yake, Black Swan hubadilisha taarifa za miamala ya kifedha
inayofanyika kwenye simu za mkononi kuwa taarifa zinazoweza kusaidia
taasisi za fedha kufanya tathmini sahihi za mikopo kwa wananchi na
wafanyabiashara wadogo ambao mara nyingi hawapo kwenye mfumo rasmi wa
benki.
Akizungumzia
mafanikio hayo, Mwanzilishi Mwenza na Afisa Mkuu Mtendaji wa Black
Swan, Derick Kazimoto, alisema kutambuliwa huko ni ishara kuwa dunia
inaanza kuona mchango wa kampuni hiyo katika kuboresha ujumuishaji wa
kifedha barani Afrika.
“Tunafurahia
kuona juhudi zetu zinatambulika kimataifa. Mamilioni ya Watanzania
wanafanya kazi na biashara kila siku lakini bado hawaonekani katika
mifumo rasmi ya fedha. Tuliianzisha Black Swan kubadilisha hali hiyo,”
alisema Kazimoto.
Alisema
teknolojia ya kampuni hiyo inachakata taarifa za kifedha kwa usalama na
kwa idhini ya watumiaji ili kusaidia wakopeshaji kufanya maamuzi ya
haraka, sahihi na yenye uwazi zaidi.
Kwa
sasa Black Swan inahudumia zaidi ya taasisi 30 za kifedha Afrika
Mashariki katika tathmini za mikopo kwenye sekta mbalimbali ikiwemo
mikopo midogo, mikopo ya kidijitali, ufadhili wa magari na mali nyingine
pamoja na huduma za kawaida za mikopo.
Miongoni
mwa bidhaa zake kuu ni “Kopa Gari”, mfumo wa kidijitali unaorahisisha
upatikanaji wa mikopo ya magari ambapo majibu ya awali ya ustahiki wa
mkopo hutolewa ndani ya dakika tano pekee.
Kampuni
hiyo pia imeanzisha mfumo wa “Manka”, unaotumia akili mnemba kusaidia
wakopeshaji kupata taarifa sahihi kuhusu uwezo wa mkopaji kulipa, hali
inayosaidia kuongeza kasi na usahihi wa utoaji wa mikopo.
Kutambuliwa
kwa Black Swan kunakuja wakati kampuni changa za teknolojia Afrika
zikiendelea kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya bara hilo kutokana na
mchango wao katika maendeleo ya uchumi wa kidijitali.
Kupitia
mafanikio hayo, Tanzania imeendelea kujijengea nafasi kwenye ramani ya
ubunifu wa teknolojia Afrika sambamba na mataifa kama Nigeria, Kenya,
Afrika Kusini na Morocco yaliyowakilishwa katika orodha hiyo ya
Bloomberg.