
TRAMEPRO imetoa mwito huo leo Julai 18,2026 katika kukimbizi ya kuzaliwa kwa Hayati Nelson Mandela aliyekuwa Rais wa nchi ya Afrika Kusini.
Taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu TRAMEPRO Tanzania Boniventura Mwalongo amesema wanaungana na mataifa ya Afrika na dunia kuadhimisha kumbukizi ya kuzaliwa kwa Hayati Nelson Mandela mmoja wa viongozi mashuhuri waliobadilisha historia ya dunia kwa kupigania uhuru, usawa, haki za binadamu na maridhiano.
Pia amesema mambo ya kujifunza kupitia kutoka kwa Nelson Mandela ni kwamba elimu ni silaha yenye nguvu zaidi ya kubadilisha dunia, msamaha ni nguvu, si udhaifu; hujenga taifa lenye umoja.
Mengine ni uvumilivu na subira vinaweza kushinda hata changamoto kubwa, Uongozi ni huduma, si nafasi ya kutawala wengine, haki na usawa ni msingi wa maendeleo endelevu.
"Mandela anatufundisha pia umoja wa Waafrika na kuheshimiana ni nguzo ya maendeleo ya bara letu. Afya, mazingira na maendeleo vinapaswa kwenda pamoja kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho, " amesema Mwalongo.
Akieleza zaidi amesema kwa waratibu asili Asili,TRAMEPRO Tanzania inaona mafunzo makubwa kutoka kwa Mandela katika kujenga umoja wa sekta, kuzingatia maadili ya taaluma, kuendeleza utafiti, kuhifadhi mimea tiba, kulinda mazingira na kushirikiana na taasisi za kisayansi ili tiba asili ichangie kikamilifu afya na maendeleo ya jamii.
Kuhusu historia ya Nelson Mandela alizaliwa Julai 18, 1918 katika kijiji cha Mvezo, Mkoa wa Eastern Cape, Afrika Kusini. Jina lake la asili, Rolihlahla, katika lugha ya Kixhosa humaanisha mtu anayetikisa tawi la mti, na kwa maana ya kawaida huashiria mtu mwenye kuhoji au kupinga hali iliyopo.
Alipoanza shule ya msingi, mwalimu wake alimpa jina la Nelson, kama ilivyokuwa desturi ya wakati huo katika shule nyingi za kikoloni.
Mandela alizaliwa katika familia ya kifalme ya kabila la Thembu. Baba yake aliitwa Gadla Henry Mphakanyiswa Mandela, aliyekuwa mshauri wa mfalme wa Thembu, na mama yake aliitwa Nosekeni Fanny Mandela.
Kutoka kwa wazazi wake alijifunza heshima, uwajibikaji, uongozi na umuhimu wa kuitumikia jamii.
Katika elimu, Mandela alianza masomo katika shule za wamisionari, akaendelea katika Chuo cha Healdtown, kisha akasoma katika Chuo Kikuu cha Fort Hare.
Baadaye alisomea sheria katika Chuo Kikuu cha Witwatersrand, ambako alijiandaa kuwa mwanasheria na mtetezi wa haki za wanyonge. Elimu yake ilimpa msingi wa kuelewa sheria na kuitumia kutetea usawa na utu wa binadamu.
Mandela aliongoza mapambano dhidi ya mfumo wa ubaguzi wa rangi (Apartheid). Kutokana na msimamo wake, alifungwa gerezani kwa miaka 27, lakini hakukata tamaa wala kuacha kuamini kuwa amani na maridhiano vinaweza kushinda chuki. Baada ya kuachiwa huru mwaka 1990, aliongoza mazungumzo yaliyoweka msingi wa Afrika Kusini mpya yenye demokrasia.
Mwaka 1994, Nelson Mandela aliingia katika historia kwa kuwa Rais wa kwanza mweusi wa Afrika Kusini aliyechaguliwa kidemokrasia. Uongozi wake ulijengwa juu ya maridhiano, msamaha na umoja wa kitaifa. Mwaka 1993, alitunukiwa Tuzo ya Amani ya Nobel kwa mchango wake katika kumaliza Apartheid kwa njia ya amani.


























































