Na Jawadu Kinyobwa WAZIRI
wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala
Bora, Ridhiwani Kikwete amewataka wahitimu wa Taasisi ya Uongozi kuwa
viongozi waadilifu, wenye nidhamu na uthubutu ili kuchangia maendeleo ya
jamii na taifa kwa ujumla.
Akizungumza Mei 15, 2026 katika
Mahafali ya Tisa ya Taasisi hiyo yaliyofanyika katika Mlimani City
jijini Dar es Salaam, Mhe. Ridhiwani alisema dunia ya sasa inahitaji
viongozi wenye maadili, uwajibikaji na uwezo wa kufanya maamuzi kwa
kuzingatia maslahi ya wananchi.
Alisema uadilifu ni sifa muhimu
ya kiongozi bora na mwenye kuaminika, hivyo wahitimu wanapaswa kutumia
maarifa na ujuzi walioupata kuwa viongozi wanaozingatia haki, uwazi na
weledi katika utekelezaji wa majukumu yao.
“Nawakumbusha umuhimu wa kuwa viongozi wenye uzalendo. Tukumbuke msemo
wa wahenga kwamba adhabu ya msaliti ni malipo ya usaliti wake. Usaliti
mkubwa katika uongozi wa umma ni sawa na ubadhirifu wa mali za umma,”
alisema Ridhiwani.
Aidha, aliwataka wahitimu hao kulinda
rasilimali za taifa na kuweka mbele maslahi ya wananchi katika maamuzi
yao ya kila siku ili kusaidia kuleta maendeleo ya kijamii na kiuchumi
nchini.
Alisema Tanzania inahitaji viongozi waaminifu na wenye
uwajibikaji ambao watatumia nafasi zao kuendeleza ustawi wa wananchi na
kuimarisha misingi ya utawala bora. 
Sambamba na hilo, Waziri
Ridhiwani alisema uongozi unaozingatia haki na uwazi utaendelea
kuitangaza vyema Tanzania pamoja na Taasisi ya Uongozi ndani na nje ya
nchi.
Awali akizungumza katika hafla hiyo, Afisa Mtendaji Mkuu
wa Taasisi ya Uongozi, Bw. Kadari Singo alisema taasisi hiyo imetimiza
miaka 15 tangu kuanzishwa kwake rasmi Julai mwaka 2010 kwa Hati ya Rais
kama Kituo cha Utaalamu wa Hali ya Juu kwa ajili ya kujenga na
kuimarisha viongozi barani Afrika.
Alisema kwa kipindi hicho,
taasisi hiyo imefanikiwa kutoa mafunzo mbalimbali ya uongozi, kuandaa
mijadala ya kisera pamoja na kufanya tafiti na machapisho yaliyosaidia
kukuza maarifa ya kiuongozi.
Kwa upande wake, akizungumza kwa
niaba ya wahitimu, Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Uwezeshaji Wananchi
Kiuchumi Zanzibar (ZEEA), Juma Burhan Mohamed alisema mafunzo hayo
yamewajengea uwezo mkubwa wa kiuongozi na kuwasaidia kufanya maamuzi
yenye tija kwa taasisi na jamii.
Alisema mahafali hayo hayakuwa
tu hitimisho la mafunzo, bali yalikuwa ishara ya mabadiliko makubwa ya
kiuongozi na maendeleo binafsi waliyoyapata ndani ya miezi sita ya
programu hiyo.


















.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)





