Dar es Salaam, Tanzania – Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameipatia Tanzania Breweries Public Limited Company (TBL) Tuzo ya Rais ya Walipakodi Bora katika Sekta ya Uzalishaji (Manufacturing), ikiwa ni kutambua mchango wa kampuni hiyo katika kukuza uchumi wa Taifa kupitia ulipaji sahihi wa kodi, uzalishaji wa ndani, uwekezaji na uundaji wa ajira.
Tuzo hiyo ilitolewa wakati wa maadhimisho ya miaka 30 ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Mlimani City, Dar es Salaam, Jumatano tarehe 1 Julai 2026.
Uamuzi wa Mheshimiwa Rais kuongoza binafsi utoaji wa tuzo hizo kwa mwaka wa pili mfululizo unaonesha umuhimu ambao Serikali inaweka katika kuhimiza ulipaji wa kodi na kutambua mchango wa sekta binafsi katika kufanikisha maendeleo ya nchi.
Kwa TBL, tuzo hii ni uthibitisho wa mchango mpana wa kampuni katika maendeleo ya Tanzania. Mbali na kulipa kodi kwa wakati na kwa usahihi, kampuni inaendelea kuchangia maendeleo kupitia ajira inazozalisha, ushirikiano wake na wakulima, wasambazaji, wafanyabiashara pamoja na jamii mbalimbali zinazozunguka shughuli zake.
Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Breweries Public Limited Company, Michelle Kilpin, alisema kuwa tuzo hiyo ni ishara ya dhamira ya kampuni ya kuendesha biashara kwa uwajibikaji na kuchangia maendeleo ya Taifa.
"Tunajivunia kupokea heshima hii kutoka kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kulipa kodi kikamilifu na kwa wakati ni wajibu wetu kama kampuni ya Kitanzania na sehemu ya mchango wetu katika maendeleo ya nchi. Tuzo hii ni ya wafanyakazi wetu, wakulima, wasambazaji, wauzaji, washirika wetu wa biashara na wadau wote katika mnyororo wetu wa thamani. Tutaendelea kuwekeza nchini na kuwa mshirika wa kuaminika katika safari ya maendeleo ya Tanzania," alisema Kilpin.
Kupitia shughuli zake za uzalishaji wa ndani, TBL inaendelea kuzalisha manufaa yanayovuka mipaka ya viwanda vyake kwa kusaidia wakulima, wasafirishaji, wasambazaji, wafanyabiashara wadogo na wa kati pamoja na wadau wengine wa biashara nchini. Aidha, kupitia ununuzi wa mazao ya ndani kama shayiri (barley) na mtama (sorghum), kampuni inachochea maendeleo ya sekta ya kilimo, kuongeza kipato cha wakulima na kuhakikisha thamani kubwa zaidi ya uchumi inabaki nchini.
Mbali na mchango wake wa kiuchumi, TBL inaendelea kuwekeza katika miradi ya uendelevu ikiwemo usimamizi wa rasilimali za maji, kuwawezesha wakulima, ununuzi wenye uwajibikaji, matumizi ya mifumo ya ufungashaji unaorejelezwa pamoja na programu za urejelezaji wa taka, hatua zinazolenga kuhifadhi mazingira na kuhakikisha matumizi endelevu ya rasilimali zinazoiwezesha kampuni kuendesha shughuli zake.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Sheria na Masuala ya Kampuni wa TBL, Neema Temba, alisema kuwa biashara yenye uwajibikaji hupimwa kwa kuzingatia utekelezaji wa sheria pamoja na athari chanya inayozalisha kwa jamii.
"Heshima hii inaakisi msingi wa maadili unaotuongoza kila siku. Tunaamini katika kufanya biashara kwa uwazi, kutimiza wajibu wetu wa kisheria na kushirikiana na Taifa ambalo limekuwa makazi ya biashara yetu kwa miongo mingi. Kampuni zinapolipa kodi stahiki, kuwekeza katika maeneo zinayofanyia kazi na kulinda rasilimali zinazowezesha shughuli zao, nchi nzima hunufaika na kusonga mbele," alisema Temba.
Tuzo hii inaongeza orodha ya mafanikio ambayo TBL imeendelea kuyapata katika maeneo ya ulipaji wa kodi, uendelevu wa biashara na uwajibikaji wa kampuni kwa jamii.
Kadiri Tanzania inavyoendelea kutekeleza agenda ya ukuaji wa viwanda na mageuzi ya uchumi, TBL imesisitiza kuwa itaendelea kuwekeza nchini, kushirikiana na jamii pamoja na kuunda thamani ya kudumu kupitia biashara inayozingatia uwajibikaji.




























































