TPSC Yaimarisha Ushirikiano wa Tanzania na Somalia Kupitia Mafunzo

 

Mkuu wa Chuo na Afisa Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dr. Ernest Mabonesho  akizungumza wakati wa   mafunzo ya kujenga uwezo watumishi wa Serikali ya Somalia  leo jijini Dar es Saam.
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope akiwa kwenye za pamoja
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope akizungmza wakati wa kufungua  mafunzo ya kujenga uwezo  kwa watumishi wa Serikali ya Somalia Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), jijini Dar es Salaam
Sehemu ya washiriki wa Mafunzo hayo.

Na Mwandishi Wetu. 

Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) imepokea ujumbe wa ngazi ya juu kutoka Serikali ya Shirikisho la Somalia kwa ajili ya mafunzo ya kujenga uwezo katika utumishi wa umma, hatua inayoonesha kuimarika kwa ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

Mafunzo hayo yanafanyika katika Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) jijini Dar es Salaam, yakihusisha watumishi kutoka Idara ya Masuala ya Baraza la Mawaziri chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu wa Somalia. Lengo kuu ni kuimarisha mifumo ya uratibu wa serikali, usimamizi wa kumbukumbu, ulinganifu wa sera na ufuatiliaji wa maamuzi.

Hafla ya ufunguzi ilihudhuriwa na viongozi waandamizi wa serikali, akiwemo Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope, aliyemwakilisha Serikali ya Tanzania.

Katika hotuba ya ufunguzi, Mkuu wa Chuo na Afisa Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dr. Ernest Mabonesho alieleza kuwa mpango huo ni hatua muhimu katika kuimarisha taasisi za umma na kuongeza ufanisi wa utendaji wa serikali. Chuo hicho, kilichoanzishwa rasmi mwaka 2000 baada ya kuunganishwa kwa taasisi za mafunzo ya utumishi wa umma, kimeendelea kuwa kitovu cha ubora katika mafunzo, utafiti na ushauri wa kiutawala.

Imeelezwa kuwa mpango huo umeandaliwa kwa ombi la Serikali ya Somalia, kufuatia majadiliano kati ya TPSC na Ofisi ya Waziri Mkuu wa nchi hiyo. Mafunzo yanajumuisha nadharia, vitendo na uzoefu wa taasisi mbalimbali, yakilenga kuwapatia washiriki mbinu zitakazoweza kutumika katika kuboresha mifumo ya utawala nchini Somalia.

Mpango huo pia umeelezwa kuwa ni matokeo ya kuimarika kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Somalia, hasa baada ya ziara ya ngazi ya juu ya Serikali ya Tanzania nchini Somalia mwezi Desemba 2025, iliyoweka msingi wa ushirikiano katika maendeleo ya sekta ya umma.

Washiriki na viongozi wamebainisha kuwa mbali na kujenga ujuzi, mafunzo hayo yanatarajiwa kuimarisha mitandao ya kitaaluma na ushirikiano wa muda mrefu kati ya nchi hizo mbili.

Hatua hii inaonesha nafasi ya Tanzania katika kusaidia maendeleo ya taasisi za umma katika ukanda huu, huku nchi mbalimbali zikiongeza juhudi za kushirikiana kuboresha utawala na utoaji wa huduma kwa wananchi.

SHARE
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment