Na Mwandishi Wetu.
MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa wa Pwani, Mariam Ibrahim, ameendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Ameyasema hayo leo alipokuwa mgeni rasmi katika mashindano ya “Mkali wa Chapati” yaliyofanyika Wilaya ya Mkuranga, Mkoa wa Pwani ambapo amefafanua mashindano hayo ni sehemu ya juhudi za kuhamasisha matumizi ya nishati safi chini ya uongozi wa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan.“Mashindano haya ni sehemu ya juhudi za kumuunga mkono Rais Dk.Samia Suluhu Hassan katika kampeni ya matumizi ya nishati safi kwa wananchi. Hakika Rais Samia ni kiongozi imara ambaye ameweka mbele maslahi ya wananchi pamoja na utunzaji wa mazingira,” amesema Mariam Ibrahim.
Aidha amewataka wananchi wa Wilaya ya Mkuranga kuachana na matumizi ya majiko ya mkaa na badala yake kutumia nishati safi kama gesi ili kupunguza ukataji wa miti na kulinda mazingira.
Pia amesema kutakuwa na mashindano mengine yajayo yakiwemo ya upishi wa pilau na nyama choma, yenye lengo la kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi pamoja na kukuza mshikamano wa kijamii.
Katika hatua nyingine, amewaomba wananchi wa wilaya hiyo kuendelea kushikamana na kushirikiana katika shughuli mbalimbali za kijamii kwa maendeleo ya jamii yao.Wakati huo huo amemshukuru Mbunge wa Jimbo la Mkuranga Abdallah Ulega, kwa kufanikisha mashindano hayo pamoja na shughuli zote zilizofanyika siku hiyo.
“Maandalizi na mafanikio ya mashindano hayo yametokana na juhudi za Mbunge Abdallah Ulega kwa kushirikiana na wananchi wa Mkuranga,”amesema.








0 comments:
Post a Comment