WEST KILI FOREST TOUR CHALLENGE 2026 KUWAKUTANISHA WANAMICHEZO NA WADAU WA UTALII


Mkuu wa Wilaya ya Siha, Dkt. Christopher Timbuka.

Na Mwandishi Wetu, Siha

Wilaya ya Siha mkoani Kilimanjaro inatarajiwa kupokea zaidi ya washiriki 800 kutoka ndani na nje ya Tanzania katika mashindano makubwa ya michezo na utalii yajulikanayo kama West Kili Forest Tour Challenge, yatakayofanyika Juni 20 hadi 21, 2026 katika ukanda wa msitu wa West Kilimanjaro.

Mashindano hayo yamezinduliwa rasmi na Mkuu wa Wilaya ya Siha, Dkt. Christopher Timbuka, aliyesema tukio hilo litakuwa chachu ya kuitangaza Siha kimataifa kupitia utalii wa asili, michezo na shughuli za kijamii zitakazochochea uchumi wa wananchi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt. Timbuka alisema mashindano hayo yatahusisha mbio za kilomita 5, 10 na 21, pamoja na mashindano ya baiskeli na pikipiki yatakayopita katika maeneo yenye mandhari ya kuvutia ya msitu wa West Kilimanjaro.

“Tunatarajia kupokea washiriki wengi kutoka sehemu mbalimbali za Tanzania na nje ya nchi. Hii ni fursa kubwa kwa Siha kuendelea kujitangaza kama kitovu cha utalii wa michezo na uhifadhi wa mazingira,” alisema Dkt. Timbuka.

Aliongeza kuwa maandalizi yote muhimu yamekamilika ili kuhakikisha mashindano hayo yanafanyika kwa mafanikio makubwa huku yakitoa nafasi kwa wananchi kunufaika kupitia biashara mbalimbali zikiwemo malazi, chakula, usafiri na huduma nyingine za kijamii.

Kwa mujibu wa waandalizi, kabla ya siku ya mashindano kutafanyika mkesha maalumu wa burudani utakaojumuisha shughuli za kijamii, muziki, chakula na vinywaji kwa washiriki na wadau mbalimbali.

Mashindano hayo yanaungwa mkono na kampuni ya Mati Super Brands Ltd ambayo imeahidi kushirikiana kuhakikisha tukio hilo linakuwa la kipekee na lenye mafanikio makubwa.

Akizungumza kuhusu malengo ya mashindano hayo, Mratibu wa West Kili Forest Tour Challenge, Bw. Mensier Elly, alisema tukio hilo si la michezo pekee bali ni jukwaa muhimu la kutangaza vivutio vya utalii vya West Kilimanjaro na kuhamasisha uhifadhi wa mazingira kupitia michezo na utalii endelevu.

“Tunataka kutumia michezo kama njia ya kuhamasisha jamii kuthamini mazingira na wakati huo huo kuitangaza West Kilimanjaro kwa dunia,” alisema Bw. Elly.

Mashindano hayo yanatarajiwa kuwa miongoni mwa matukio makubwa ya michezo na utalii nchini mwaka huu kutokana na ushiriki mkubwa unaotarajiwa pamoja na mvuto wa kipekee wa mazingira ya West Kilimanjaro.



Mbunge wa Jimbo la Siha mkoani Kilimanjaro, Dkt. Godwin Mollel akitoa neno.

Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti West Kilimanjaro, PCO Robert Faida akisoma risala. 

 Mratibu wa West Kili Forest Tour Challenge, Bw. Mensier Elly 


















Mmoja ya Wazee wa Siha akitoa neno.










SHARE
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment