Profesa Muhongo akerwa na ufaulu duni wa wanafunzi jimboni kwake

Mbunge wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amesema amesikitishwa na matokeo ya Kidato cha Nne katika jimbo lake na kusisitiza umuhimu wa kuchukua hatua za haraka ili kukomesha hali hiyo.

Aliyasema hayo hivi karibuni katika kijiji cha Murangi, Mkoani Mara kwenye hafla ya kukabidhi gari la kisasa la wagonjwa la Kituo cha Afya cha Murangi.
Alisema shule za Serikali jimboni humo zimetia aibu kwani matokeo yao hayaridhishi na sio ya kujivunia na huku akisisitiza hatua za haraka zinahitajika ili kubaini chanzo cha tatizo hilo la wanafunzi wengi kufanya vibaya kwenye mitihani yao.
Kufuatia hali hiyo, Profesa Muhongo aliagiza wasaidizi wake watano ambao waliajiriwa mapema mwaka huu maalum kwa kafuatilia shughuli za jimbo kutembelea shule zilizopo kwenye maeneo yao na kuzungumza na wakuu wa shule hizo na kumpatia taarifa.
Aliagiza wakutane na wakuu wa shule zote zilizomo jimboni humo na kila mkuu wa shule aeleze sababu za kuwa na matokeo mabaya ya mitihani iliyopita ya kidato cha nne.
“Hawa vijana nimewaajiri kufuatilia shughuli za jimbo na kwa kawaida kila wiki wananiletea taarifa za masuala mbalimbali ya kimaendeleo ambayo ninatekeleza ili kuelewa kuhusu utekelezaji wake,” alisema.
Alisema binafsi anaelelewa baadhi ya sababu zinazochangia wanafunzi kufanya vibaya lakini ametoa agizo hilo la kupata maelezo ya wakuu wa shule ili kujiridhisha zaidi.
Mbali na hilo, Profesa Muhongo aliwalaumu madiwani jimboni humo kwa kushindwa kufuatilia suala la elimu. “Madiwani hii ni kazi yenu, haiwezekani tumepata matokeo mabaya na hadi leo hii hamjaitisha kikao kujadili.”
Aliagiza kwamba taarifa husika ikamilike ndani ya mwezi mmoja na baada ya kupatiwa taarifa hiyo alisema ataitisha mkutano maalum wa elimu ili kuijadili.
Alisema endapo kutathibitika kuna wanaosababisha hali hiyo ya matokeo mabaya kwa namna yoyote ile watu hao itabidi wapewe adhabu.
Alisema inawezekana baadhi ya wazazi pia kwa namna moja ama nyingine wanachangia vijana kupata matokeo mabaya. “Hadi sasa kwa taarifa nilionayo kuna vijana 224 wamefaulu kujiunga na kidato cha kwanza lakini hadi hivi sasa hawajajiunga; na madiwani mpo tu mnatazama bila kuchukua hatua na mnaona ni kawaida,”
Aliagiza kupatiwa majina ya wazazi wote waliogoma kuruhusu watoto wao kuendelea na masomo na vilevile yapelekwe kwa Mkuu wa Wilaya. “Nataka hili lifanyike ndani ya wiki moja na watoto wote wawe wameenda shule.”
Vilevile Profesa Muhongo alisema suala alilogundua ni kwamba wanafunzi wengi hawana mazoea ya kujisomea vitabu ili kuongeza uelewa baada ya kutoka shule.
Alisisitiza umuhimu wa kusoma vitabu badala ya kukariri madaftari ya darasani. “Unakuta motto anatoka shule halafu anasoma daftari aliloandika darasani badala ya vitabu. Ndiyo maana nimewaletea vitabu ili kuwa na uelewa mpana zaidi.”
Alisema awamu ya kwanza alipeleka vitabu 7,110 vya Sekondari na vitabu 12,800 vya msingi na awamu inayofuata vitabu vitakavyoingia vitakua zaidi ya 25,000 vingi vikiwa ni vya sayansi, hesabu na kiingereza.
Mbali na hilo, Profesa Muhongo alihoji utendaji wa Halmashauri na kueleza kutoridhishwa na utendaji wake na hivyo aliagiza kufuatiliwa kwa karibu kwa Afisa Elimu wa Halmashauri hiyo.
“Inashangaza Halmashauri nao wanalalamika sasa kazi yao nini?; Afisa Elimu hafai, tutamfuatilia kwa karibu,” alisema.
Profesa Muhongo vilevile aliagiza madiwani wote jimboni humo kuacha kuingilia shughuli za watendaji hususan kwenye suala la ukusanyaji wa kodi.
“Hakuna diwani kukusanya kodi, nyie ni wa kupokea taarifa kujadili na kufanya tathmini; ni utendaji wa hovyo diwani kujihusisha na ukusanyaji kodi. Mliomba udiwani kuleta maendeleo na siyo kutumbua maisha,” alisisitiza.
Hafla hiyo ya makabidhiano ilihudhuriwa na wananchi mbalimbali wa jimboni humo, wataalamu wa afya wa kituo cha Murangi, wadau wa maendeleo na watendaji wa Halmashauri husika.
 Mbunge wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kulia) akitoa maagizo kwa wasaidizi wa Ofisi zake tano za Jimbo.
Mbunge wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kushoto) akifurahia jambo na Mzee Joseph Nyangaga mkazi wa kijiji cha Makojo mara baada ya kumaliza mkutano wake na wananchi wa jimbo la Musoma Vijijini.
SHARE
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment